Jumatano, 6 Agosti 2014

BUNGE LA KATIBA LAANZA TENA....HII NI HOTUBA YA MWENYEKITI SAMUEL SITTA WAKATI WA UFUNGUZI WA AWAMU YA PILI YA BUNGE HILO



Karibuni tena Dodoma Waheshimiwa Wajumbe wa Bunge Maalum la kutunga Katiba ya nchi yetu. Sote tuna kila sababu ya kumshukuru Mwenyezi Mungu wetu kwa kuendelea kutupa uhai na afya hadi leo kutuwezesha kuwepo ndani ya ukumbi huu.

Tupo humu ili tuitekeleze kazi waliyotukabidhi Watanzania wenzetu milioni arobaini na sita (46) ya kuwapatia Katiba mpya. Dhamana hii ni nzito na haistahili kufanyiwa ajizi.

Tunaendelea na shughuli zetu za Bunge Maalum kwa kuzingatia Kanuni ya 30 (1) inayosema:

"Akidi kwa kila kikao cha Bunge Maalum isipokuwa wakati wa kupitisha uamuzi wa Bunge Maalum itakuwa ni nusu ya Wajumbe wote wa Bunge Maalum".

Nimetaarifiwa na Katibu kwamba wajumbe waliokuja Dodoma kuhudhuria ni zaidi ya robo tatu ya Wajumbe wote wa Bunge Maalum. Nawashukuruni nyote kwa kuja hapa Dodoma ili kutimiza wajibu wenu.

Kwa niaba yenu, nawashukuru Watanzania wenzetu wote ambao kwa mamilioni wamedhihirisha utashi mwema wa kisiasa kwa kuunga mkono hatua ya Bunge Maalum kuendelea na kazi zake hadi tuipate Katiba inayopendekezwa ambayo wataipigia kura ya maoni.

Kipekee na kwa niaba yenu, nawashukuru kwa dhati viongozi wetu wa dini wa madhehebu yote wanaloliombea Taifa hili mafanikio Bunge Maalum, wakitanguliza utaifa pamoja na amani ya nchi na umoja ndani ya nchi na siyo ubinafsi na maslahi ya makundi.

Kwa leo sikupenda sana kuzungumzia hoja mbali mbali zinazotawala magumzo ya mchakato wa Katiba mpya hapa nchini, magumzo yanayoendeshwa na makundi maalum kwa jazba na hata matusi.

Hata hivyo nalazimika kutoa maelezo ya ufafanuzi kuhusu upotoshaji mkubwa unaoendeshwa na baadhi ya watu kuhusu Bunge Maalum. Nikiwa Mwenyekiti wenu ninao wajibu wa kuwafafanulia wananchi kuhusu uhalali wa shughuli za Bunge Maalum linaloendelea na utaratibu wa shughuli zetu.

Ni Rasimu ya Tume au la
Wapo wanaodai kuwa eti hapa Bungeni hatujadili Rasimu ya Tume. Tuhuma hii haina ukweli hata kidogo. Msingi wa majadiliano yote tangu tumeanza ni Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume ya Katiba.

Utaratibu ni kwamba pale ambapo wajumbe wanaona panafaa kurekebishwa wanafanya hivyo. Maana ya rasimu ni andiko ambalo halijajitosheleza bila kupata ithibati ya taasisi ya juu zaidi.

Anayekabidhiwa rasimu anayo haki na mamlaka ya kuirekebisha. Vinginevyo kujadili rasimu hakuna sababu.

Itakuwa ni jambo la ajabu na lisilo na mantiki yoyote kuwa taasisi iliyopewa mamlaka ya kujadili Rasimu ikishaijadili iiache ibaki kama ilivyokuwa wakati ilipowasilishwa!

Je suala ni muundo wa Muungano tu?
Maudhui ya Rasimu yanajumuisha baadhi ya masuala muhimu yafuatayo:

-Kuimarisha Muungano wetu kwa kuleta uwiano     bora zaidi wa mamlaka ya Zanzibar na Tanzania      Bara ndani ya Muungano

-Kuimarisha haki za binadamu ili kuwawezesha      raia wa kawaida kufaidi uhuru wa demokrasia     bila ubabe na dhuluma

-Kuzuia wachache kufuja rasilimali za taifa bila       kujali maslahi ya wengi na ya vizazi vijavyo.

-Kujenga uwiano sahihi na wenye haki baina ya      wanawake na wanaume katika nafasi za uongozi.

-Kubainisha hatua zenye kuleta matumaini mapya ya maendeleo kwa makundi maalum ya vijana     wakulima wadogo, wafugaji, wafanyakazi wa ngazi   za kawaida, walemavu, wafanya biashara wadogo   na wajasiriamali wengine.

-Kuweka msingi imara wa kutungwa kwa sheria      kakamavu za kuzuia ukandamizaji wa raia,        unyonyaji, wizi wa mali ya umma, rushwa,    hujuma dhidi ya uchumi na kuzuia mapato        haramu na fedha chafu.

-Kutambua haki za ardhi kwa wakulima, wafugaji    na wajasiriamali wengine ili kupunguza migongano na migogoro.

-Kuweka Misingi ya utawala bora inayozingatia        uadilifu, sifa stahiki na ufanisi.

-Kuwezesha kutungwa kwa sheria bora zaidi     zitakazosimamia chaguzi zilizo za haki na huru    zaidi pamoja na kuwepo Tume za Uchaguzi       zilizoboreshwa.

Zaidi ya hivyo, yapo mapungufu katika Rasimu iliyopo kwa kuachwa masuala ya kuwezesha Serikali za mitaa; kutoa maelekezo kuhusu masuala ya matumizi ya ardhi na rasilimali nyingine za Taifa. Nini kinatuzuia kuiboresha Rasimu kwa kuyaongeza mambo haya ndani ya Katiba kwa faida ya Taifa?

Yote haya ni masuala muhimu ambayo yamo ndani ya rasimu na wakati wake wa kuyaweka sawa ndiyo huu. Pamoja na umuhimu wake suala la muundo wa Muungano si suala la kutulazimisha tuyaahirishe mazuri yote yaliyomo katika Rasimu tuliyopewa.

Uhalali wa Shughuli za Bunge Maalum
Pamoja na uhalali wa kisheria wa Bunge hili Maalum kuendelea kufanya kazi zake, linao pia uhalali wa kisiasa kutokana na sifa za uwakilishi wetu na pia maudhui yaliyomo ndani ya Rasimu. Kutofautiana maoni hakuwapi hadhi tofauti baadhi ya wajumbe kujiona wao wana uhalali zaidi mbele ya wananchi kuliko wenzao.

Ndiyo maana utaratibu umewekwa wa kupiga kura na wa maridhiano. Utamaduni mpya unaoanza kujengwa na baadhi ya viongozi wa jamii wa kususia mijadala halali na kwenda nje kuelezea hoja za upande mmoja hauna nafasi katika Tanzania jamii isiyotaka fujo na utengano.

Wajumbe wa Bunge Maalum wanaoendelea na kazi mjini Dodoma ni wateule wa Rais kwa niaba ya wananchi kwa kazi ya kutunga Katiba. Kazi hii haiwezi kusitishwa kwa sababu tu wajumbe wachache wameisusia. Tutazingatia matakwa ya sheria katika kufikia hatma ya mchakato wa Katiba.

Mabadiliko ya Kanuni
Kama nilivyoeleza hapo mwanzo, Rasimu ina jumla ya sura kumi na saba (17) zenye mambo mengi yenye maslahi kwa Watanzania wote. Kwa muda tuliopewa wa siku sitini (60) isingewezekana kuikamilisha kazi tuliyopewa ndani ya muda. Ikumbukwe kwamba kwa Kanuni zilivyo, kila sura mbili zinahitaji siku tisa kuzifanyia kazi.

Kwa njia hiyo, ingetuchukua siku takriban mia moja thelathini (130) ili kuikamilisha kazi hii! Pendekezo la msingi hapa ni kwamba Kamati zetu kumi na mbili (12) zizingatie na kuzijadili sura kumi na tano (15) za Rasimu na pia zikamilishe uandishi wa sura mbili zilizojadiliwa awali na ikibidi ziongeze sura ambazo zitadhihirika kuwa ni muhimu.

Naamini mtiririko huu utatuwezesha kuwa na mpangilio bora zaidi wa sura na ibara katika Katiba mpya. Tusingependa na wala isingefaa kuomba tena muda wa ziada wa kazi ya Katiba ndio maana tunafanya mabadiliko ya Kanuni.

Kamati ya Uongozi iliyoketi Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2014 imependekeza yafanywe mabadiliko ya Kanuni za Bunge Maalum kuwezesha kazi ikamilike ndani ya muda tuliopewa.

Kwa hiyo nitawaomba tuyatafakari mapendekezo ya mabadiliko ya Kanuni na hatimaye kuyapitisha ili ratiba ya kazi zetu iende sawa. Nitawaomba muikubali ratiba iliyogawanywa leo na pia mkubali kuzibadilisha Kanuni kwa lengo nililolieleza hapa.

HITIMISHO
Pamoja na maoni ya kila namna yanayoendelezwa kujadili mchakato wa Katiba nje ya Bunge hili, ni muhimu wahusika wapunguze jazba, chuki na upotoshaji. Bunge Maalum lisaidiwe kwa mawazo chanya ili limalize kazi yake.

Sisi tuliomo humu katika Bunge Maalum tuna wajibu wa kuifanya kazi yetu kwa umakini na kwa uadilifu ili kazi yetu iwe bora. Tujadiliane kwa uungwana. Tofauti za mawazo zisitufanye tuingize chuki na maneno yasiyofaa.

Katika mabadiliko ya Kanuni nashukuru sasa Kiti kimepewa mamlaka ya kushughulikia utovu wa nidhamu ndani ya wakati. Lakini ninaamini haitakuwa lazima kwangu mimi au Makamu Mwenyekiti kutumia nguvu za mamlaka yetu ila tu pale itakapobidi.

Nawatakia nyote Mkutano wenye mafanikio kwa maslahi mapana ya nchi yetu.

MUNGU IBARIKI TANZANIA!
Samuel Sitta - MB
MWENYEKITI BUNGE MAALUM LA KATIBA

MJUMBE WA UKAWA ATINGA BUNGENI




Wakati wajumbe wa Bunge la Katiba wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) wakiendelea na msimamo wa kususia vikao vinavyotarajiwa kuanza leo mjini Dodoma, mmoja wa wajumbe wake jana aliripoti bungeni na kujiandikisha. 
Mjumbe huyo, Clara Mwatuka ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalumu (CUF), alionekana katika Viwanja vya Bunge saa 6:30 mchana akiwa ameongozana na wabunge kadhaa wa CCM wakiwamo Livingstone Lusinde (Mtera) na Jerome Bwanausi (Lulindi).
CUF ni moja ya vyama vinavyounda Ukawa, pamoja na Chadema na NCCR Mageuzi na tayari viongozi wakuu wa vyama hivyo, Profesa Ibrahim Lipumba, Freeman Mbowe na James Mbatia wametangaza kwamba wajumbe wote wanaotokana na umoja wao hawatashiriki vikao vya Bunge hilo.
 
Mwatuka baada ya kujaza fomu maalumu za kujiandikisha, alielekea lango la Magharibi na kuingia kwenye gari la Bwanausi.
Awali, alipoulizwa kwenye Viwanja vya Bunge kuhusu kuwapo kwake Dodoma, alikataa kuzungumza lakini alikiri kujiandikisha bungeni.
 
Baadaye alipoulizwa imekuwaje akajiandikisha ilhali uongozi wa chama chake umesema hawatashiriki, Mwatuka alijibu: “Kwa hapo ni mapema sana kuzungumzia suala hilo, nitazungumza kesho (leo) kule bungeni ukinitafuta.”
 
Hata hivyo, baada ya dakika kama 30 kupita, Mwatuka alimpigia simu mwandishi na kumwambia: “Sasa kuhusu mimi kuja Dodoma, ni kweli kwamba niko hapa maana nasomesha na nilipofika nimeamua kwenda pale bungeni kuripoti.”
 
Aliogeza: “Ila mimi pamoja na kujiandikisha, sitashiriki vikao vya Bunge mpaka hapo tutakapokuwa tumepewa mwongozo, maana tuliambiwa kwamba majadiliano yanaendelea kwa hiyo tukiruhusiwa nitakwenda, vinginevyo sitashiriki kabisa, ndiyo hivyo.”
 
Bwanausi kwa upande wake alisema alimpa lifti Mwatuka kutoka Dar es Salaam baada ya mbunge huyo wa CUF kuomba msaada wa usafiri kwenda Dodoma.
 
“Ni jambo la kawaida, tulionana Dar es Salaam na akaniuliza iwapo ninakwenda Dodoma na mimi kweli nafasi ilikuwapo kwenye gari, kwa hiyo tumekuja naye hadi hapa, sasa zaidi ya hapo mimi sifahamu,”alisema.
 
Wajumbe kutoka Zanzibar na wale wa kundi la 201 ndiyo waliokuwa wengi katika usajili wa jana na wajumbe ambao wanatokana na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hasa kutoka Tanzania Bara wakionekana wachache.
 
Milango yote ya kuingia katika eneo la Bunge ilikuwa imefungwa na kuacha lango moja tu la Magharibi, hali iliyosababisha baadhi ya wajumbe kuhangaika hadi pale walipopata msaada wa polisi waliokuwa wakilinda

Mkutano wa Bunge Maalumu ambao unafanyika kwa mara ya pili, unatarajia kuchukua miezi miwili ambayo wajumbe wake wanapaswa kuitumia kukamilisha kazi ya kupitia sura 15 za Rasimu ya Katiba zilizosalia na kupiga kura kuamua kuhusu sura mbili zinazohusu Muungano.
 
Katika mkutano uliomalizika Aprili mwaka huu, wabunge walikuwa wametumia zaidi ya siku 70 na walifanikiwa kupitia sura ya kwanza na sita ambazo hata hivyo, hazikupigiwa kura.
 
Hadi jana jioni Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samuel Sitta alikuwa akiongoza kikao cha Kamati ya Uongozi, lakini hakukuwa na taarifa rasmi kuhusu ratiba wala ajenda za mkutano unaotarajiwa kuanza leo.
 
Wabunge wapata ajali
Katika tukio jingine, Mbunge wa Tabora Mjini, Ismail Aden Rage na Mbunge wa Viti Maalumu, Munde Tambwe wamenusurika kifo baada ya gari walilokuwa wakisafiria wakati wakitokea Tabora kwenda Dodoma kupata ajali.
 
Wabunge hao wamelazwa katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma na hali zao zilikuwa zinaendelea vizuri.
 
Akizungumza akiwa katika Wodi Namba 18, Rage alisema amepata majeraha katika bega la kushoto na eneo la nyuma ya mgongo baada ya dereva wa gari walilokuwa wakisafiria kujaribu kulipita lori lililokuwa mbele yao, lakini ghafla lori hilo likaingia katikati ya barabara.
 
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Ezekiel Mpuya aliwataja majeruhi wengine wa ajali hiyo iliyotokea katika eneo la Chigongwe, Dodoma kuwa ni Issa Chimwaga (31), Mwanahamisi Ramadhani (34) na dereva John Hoya (32) ambaye hakuuumia.
 
Alisema vipimo vimeonyesha kuwa mbali na kupata majeraha usoni na kichwani, Munde pia amevunjika mkono wakati Rage ameteguka bega la kushoto.